Tuesday, January 22, 2013

Mwanafunzi wa sekondari ajinyonga kwa mtandio

MWANAFUNZI wa kidato cha tatu wa Shule ya Sekondari Mbezi Inn, Daines Richard (15) amekutwa chumbani kwake akiwa amejinyonga kwa mtandio aliokuwa ameutundika darini. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela amesema tukio hilo lilitokea Januari 18 mwaka huu Mbezi Kimara.

Alisema sababu ya kujinyonga inasadikiwa kuwa ni baada ya baba yake kumwambia aoshe vyombo na yeye alikataa hali iliyosababisha mzozo kati yake na baba yake.

Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Tumbi Kibaha na upelelezi unaendelea.

Wakati huo huo, moto umezuka ghafla katika maeneo ya Kigogo Mkwajuni kwenye nyumba ya Protas Ernest (33) na kuteketeza chumba kimoja katika nyumba ya vyumba vinne pamoja na vitu vyote vilivyokuwamo ndani.

Kenyela alisema tukio hilo lilitokea Januari 18 mwaka huu na inasadikiwa kuwa chanzo cha moto huo ni mshumaa uliowashwa na mwenye nyumba.

Moto huo ulizimwa na Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji cha Jiji kwa kushirikiana na wananchi wa eneo hilo.

Alisema thamani ya mali zilizoteketea kwa moto bado haijafahamika na hakuna madhara yoyote kwa binadamu.

No comments:

Post a Comment