Saturday, December 22, 2012

Azinduka Toka Kwenye Jeneza Aomba Maji ya Kunywa Afariki Tena



NewsImages/6458802.jpg
Mtoto Kelvin enzi za uhai wake
Monday, June 11, 2012 2:51 AM
Mtoto wa miaka miwili wa nchini Brazili alizinduka toka kwenye jeneza ambalo mwili wake uliwekwa kwaajili ya kuagwa, alimuomba baba yake maji ya kunywa kabla ya kujilaza tena chini na kufariki tena.
Katika tukio ambalo ni vigumu sana kuamini kuwa linaweza kuwa kweli ingawa limetokea kweli, mtoto mmoja wa nchini Brazili aliyejulikana kwa jina la Kelvin Santos alizinduka toka kwenye jeneza na kumuomba baba yake maji ya kunywa kabla ya kufariki tena.

Gazeti la ORM la nchini Brazili limeripoti kuwa Kelvin aliwahishwa hospitali katika mji wa Belem kaskazini mwa Brazili alipozidiwa kwa ugonjwa wa pneumonia.

Alitangazwa kuwa amefariki baada ya kusimama kupumua kwenye majira ya saa mbili kasoro usiku wa siku ya ijumaa. Mwili wake ulikabidhiwa kwa wazazi wake ukiwa ndani ya mfuko wa plastiki.

Taratibu za mazishi zilianza ambapo mwili wake uliwekwa kwenye jeneza lililoachwa wazi juu ili ndugu na jamaa watoe heshima zao za mwisho.

Lisaa limoja kabla ya mazishi kufanyika siku ya jumamosi, Kelvin alinyanyuka toka kwenye jeneza na kukaa na kumwambia baba yake "Baba naomba maji ya kunywa".

Baba yake Kelvin aliyetajwa kwa jina la Antonio Santos, alisema "Kila mtu alianza kupiga kelele, hatukuamini macho yetu, tulidhani miujiza imetokea na mtoto wetu amerudi tena duniani".

Hata hivyo furaha hiyo ya mshtuko wa kumuona Kelvin amezinduka haikudumu sana kwani Kelvin alijilaza tena chini kama alivyokuwa amelazwa mwanzo.

"Hatukuweza kumzindua tena, alifariki tena kwa mara nyingine", alisema baba wa mtoto huyo.

Santos alimchukua mwanae na kumwahisha tena hospitali ambako madaktari walimchunguza tena Kelvin na kuthibitisha kuwa Kelvin haonyeshi dalili ya uhai.

"Walinithibitishia kuwa mtoto wangu amefariki lakini hawakutoa maelezo yeyote kwanini mwanzo alizinduka alipotangazwa amefariki", alisema baba wa mtoto huyo.

Familia ya Kelvin iliamua kuahirisha mazishi kwa zaidi ya lisaa limoja kwa matumaini huenda akazinduka tena lakini ilipofika mida ya saa 11 jioni waliamua kumzika.

Kwa kuhofia kuwa mtoto wake atakuwa amefariki kutokana na matibabu duni aliyopewa mwanzoni alipowahishwa hospitali baba wa mtoto huyo amefungua kesi polisi ambapo uchunguzi wa tukio hilo umeanzishwa.

No comments:

Post a Comment